Wednesday 1 July 2015

#MAGAZETINI JULY1..Maiti yatoa jasho na kutikisika, Bei ya Petrol haishikiki na kidato cha 5 wakosa nafasi.

LAYIII

HIGHMTANZANIA
Hali ya sintofahamu imeibuka katika eneo la Magomeni, Wilaya ya Bagamoyo baada ya mwili wa marehemu Hatujuani Shaaban kushindikana kuzikwa kutokana na ndugu zake kudai ulikuwa ukitokwa jasho, kutingisha miguu, kichwa na mikono wakati ukitayarishwa kwa maziko.
Kutokana na hali hiyo mwili huo ambao ulikuwa uzikwe jumapili uliachwa hadi jana baada ya daktari kuitwa na kuishauri familia, ndipo zoezi la mazishi likafanyika.

Hatujuani alifariki dunia katika hospitali ya Wilaya ya Bagamoyo jumapili saa mbili asubuhi na mwili wake kukabidhiwa kwa ndugu zake kwa ajili ya taratibu za mazishi.
Ndugu yake aitwaye Mlau Mzee alisema walipofika nyumbani maandalizi ya mazishi yalianza kufanyika kwa taratibu za dini ya kiislamu na walitarajia kuuzika siku hiyo hiyo ya jumapili.
Alisema taratibu za kuosha mwili wa marehemu zilishindikana  kutokana na maiti hiyo kujinyoosha, kutikisa kichwa na mguu wa kulia hali iliyowafanya wasitishe zoezi hilo na kumwita daktari.
Mzee alisema baada ya mwili huo kaachwaa juzi, hatimaye jana waliamua kumsafisha tena ambapo marehemu alitikisa tena mkono na ndugu kuamua kuwaita waganga wa kienyeji.
Daktari msadizi wa hospitali ya Wilaya ya Bagamoyo Ally Ponza alikiri kutokea kwa kifo cha mtu huyo baada ya kumpokea akiwa na malaria kali na baadaye alifariki.
Alisema alipigiwa simu na muuguzi kuwa mama huyo amefariki na yeye kwenda kumpima na kuhakikisha amefariki kabla ya kuwaambia ndugu zake.
MTANZANIA
Mbunge wa Igunga Peter Kafumu na Naibu Waziri wa Nishati na madini  Charles Mwijage nusura wazichape jana bungeni baada ya kurushiana maneno makali bungeni.
Tukio hilo lilitokea wakati wa semina ya kujengewa uelewa kuhusu miswada mitatu iliyotarajiwa kuwasilishwa kuanzia leo hadi Julai 6 kwa hati ya dharura.
Miswada hiyo ni sheria ya Petrol, usimamizi wa mapato ya mafuta na muswada wa sharia ya uwazi na uwajibikaji katika tasnia ya uchumbaji Tanzania ya mwaka 2015.
Dk.Kafumu akichangia alisema sheria hizo zinahitaji muda ili zitazamwe vizuri na kwamba zikiharakishwa zitasababisha matatizo makubwa.
Kauli hiyo ilisababisha Mwijage kutaka kumpiga Mbunge huyo baada ya kuwapo kwa majibizano makali kati yao.
Mwijage alinyanyuka na kumnyooshea kidole Kafumu kwa ukali huku akizungumza maneno ambayo hayakusikika na tafrani hiyo iliendelea kwa muda huku baadhi ya Wabunge wakimzoe Naibu Waziri huyo.
Mwenyekiti wa kamati ya Bunge Richard Ndassa alimwamuru Mwijage akae chini na ajiheshimu kwa kuwa ndani ya ukumbi huo kulikuwepo na bosi wake ambaye ni Waziri Nishati na Madini George Simbachawene.
“Mhe. Waziri ongea na kiti na sio Mbunge, na usimnyooshee mwenzako kidole, na ukumbuke wewe ni Naibu Waziri na Waziri wako yuko hapa”Ndassa.
JAMBOLEO
Wabunge wanatarajia kupata mafao yao kuanzia Jula 10 baada ya Jakaya Kikwete kuvunja Bunge Julai 9 mwaka huu, Dodoma.
Wabunge wametoa mapendekezo ya kutaka kuongezewa mafao yao ya hitimisho la Bunge la 10, ambapo sasa kila Mbunge atalipwa kiasi cha zaidi ya milioni 238 na kwa idadi ya Wabunge wote Hazina itapaswa kuwalipa wabunge jumla ya shilingi 85,024,548,,000.
Kaimu katibu wa Bunge Kitolina Kippa alisema mafao ya Wabunge yatatolewa baada ya Bunge kuvunjwa iwapo Hazina itakuwa imekamilisha utaratibu mzima wa malipo hayo.
Alisema kwa sasa bunge linaendelea na vikao vyake na kukana taarifa za Wabunge kutaka kulipwa mafao hayo ijumaa kabla ya bunge kumalizika.
“Sijapata taarifa za Wabunge kutaka kulipwa gedha zao Ijumaa, ila natambua kuwa watalipwa baada ya kuvunjwa kwa Bunge hilo, kwani ndio utumishi wao utakuwa umefikia kikomo” Kippa.
MWANANCHI
Serikali imepandisha bei ya mafuta kuanzia leo baada ya jiji la Dar es Salaam kukumbwa na uhaba wa muda wa nishati hiyo kutokana na baadhi ya wafanyabiashara kusitisha mauzo kusubiri kunufaika na bei mpya.
Mamlaka ya Udhibiti wa Hudama za Nishati na Maji (EWURA) ilitangaza jana kuwa kuanzia leo bei ya petroli imepanda kwa Sh232 kutoka bei ya sasa ya Sh1,966. Bei ya kikomo ya petroli sasa itakuwa Sh2,198, ikiwa ni ongezeko la asilimia 11.82.
Bei ya dizeli imepanda kwa Sh261, ikiwa ni ongezeko la asilimia 14.65 na hivyo bei mpya itakuwa Sh2,043 badala ya Sh1,782, wakati mafuta ya taa yamepanda kwa Sh369 sawa na asilimia 22.75.
Tangu bei ya mafuta ghafi ishuke hadi chini ya Dola 50 za Marekani kwa pipa mapema mwaka huu na kusababisha bei ya petroli kushuka hadi Sh1,652 mwezi Machi, mwenendo wa bidhaa hiyo imekuwa ni kupanda.
Hadi jana, mafuta ghafi duniani yalikuwa yanauzwa chini ya Dola 60 za Marekani kwa pipa katika soko la dunia, lakini nishati hiyo nchini imerejea kwenye bei ambayo mafuta ghafi yalikuwa yakiuzwa Dola 100 kwa pipa.
Mkurugenzi mkuu wa Ewura, Felix Ngamlagosi alisema mabadiliko aliyotangaza yanatokana na bei ya mafuta katika soko la dunia, pia kuendelea kudhoofika kwa thamani ya shilingi dhidi ya Dola ya Marekani pamoja na mabadiliko ya tozo za Serikali katika mafuta kuanzia Julai Mosi, 2015.
Alisema thamani ya shilingi kwa machapisho ya bei za Juni na Julai 2015, imepungua kwa Sh 175.11 dhidi ya dola ya Marekani sawa na anguko la asilimia 8.65.
“Juni mwaka huu bei za jumla petroli ziliongezeka kwa Sh232.35 kwa lita sawa na asilimia 12.49, dizeli Sh261.15 kwa lita sawa na asilimia 15.57 na mafuta ya taa Sh369.41 kwa lita sawa na asilimia 24.32,”Ngamlagosi.
Pamoja na naibu waziri wa Nishati na Madini, Charles Mwijage kutoa tamko kali bungeni kuonya wafanyabiashara dhidi ya vitendo vya kutouza mafuta, baadhi ya vituo vilikuwa havitoi huduma jana na juzi.
Ewura ilisema jana inamfuatilia mtu aliyesambaza ujumbe kwa njia ya mitandao ya kijamii kutaarifu kuwapo kwa njama za wafanyabiashara kutouza mafuta kwa siku mbili kusubiri bei mpya.
Ngamlagosi alisema Ewura imeiandikia barua Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) na Jeshi la Polisi kutaka wachunguze kujua ujumbe huo ili muhusika achukuliwe hatua.
“Upungufu wa mafuta uliojitokeza mkoani Musoma na kuwasababishia usumbufu wananchi tunafuatilia na tukibaini watapewa adhabu ya kulipa faini ya Sh20 milioni au kwenda jela au kufutiwa leseni ya biashara ya mafuta,” Ngamlagosi.
MWANANCHI
Wanafunzi 18,751 waliofaulu mtihani wa kidato cha nne mwaka 2014, wamekosa nafasi ya kujiunga na shule za kidato cha tano kwa sababu mbalimbali ikiwamo ufinyu wa nafasi.
Kati ya hao, wanafunzi 479 wamechaguliwa kujiunga na vyuo vya ufundi huku idadi ya wanafunzi wa kike waliochaguliwa kujiunga na vyuo hivyo ikiongezeka kwa asilimia 25 kutoka wanafunzi 117 mwaka 2014 mpaka kufikia wanafunzi 147 mwaka huu.
“Baadhi ya wanafunzi wamekosa nafasi kutokana na umri mkubwa na baadhi ya watahiniwa wa kujitegemea wanakosa sifa za kuchaguliwa,” Naibu Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (TAMISEMI), Kassim Majaliwa alisema hapa jana alipokuwa akitangaza kuchaguliwa kwa wanafunzi hao.
Alisema wanafunzi 55,003 sawa na asilimia 74.5 ya wanafunzi 73,754 waliofaulu mtihani wa kidato cha nne mwaka jana ndiyo waliochaguliwa kujiunga na kidato cha tano.
Majaliwa alisema kuna ongezeko la ufaulu la wanafunzi 918 mwaka huu, ikilinganishwa na wanafunzi 54,085 waliochaguliwa mwaka 2014 kujiunga na kidato cha tano.
Alisema wanafunzi waliokosa nafasi kuingia kidato cha tano watadahiliwa na Baraza la Taifa la Ufundi (Nacte) kwenye fani mbalimbali kama vile ualimu, afya, maendeleo ya jamii na kilimo.
Alisema ufaulu wa watahiniwa wa kidato cha nne mwaka 2014 kuanzia daraja la ‘distinction’ hadi ‘credit’, yaani ufaulu wa wastani (GPA) wa 5.0 hadi 1.6 ni watahiniwa 73,754 sawa na asilimia 37.4 ya wanafunzi 240,410 waliofanya mtihani huo.
Alisema uchaguzi ulifanyika kwa kufuata machaguo matano ya tahasusi (combinations) yaliyojazwa na wanafunzi kwenye fomu ya uchaguzi ‘Selform.’
Alisema mfumo wa kompyuta ulitumika katika kumpanga mwanafunzi katika uchaguzi wake wa masomo na shule kwa kuanzia na chaguo la kwanza. “Kama mwanafunzi atakuwa hana sifa katika machaguo yote aliyoomba, hupangiwa chaguo la somo alilofaulu zaidi na katika shule iliyopo karibu na wilaya yake ya makazi kulingana na tahasusi na nafasi zilizopo,” alisema Majaliwa.
Alisema wanafunzi 29,744 watajiunga na masomo ya sayansi na 25,259 watajiunga na masomo ya sanaa na biashara.
Aliwataka wanafunzi waliochaguliwa kuripoti katika shule walizopangiwa ili kuanza muhula wa kwanza wa masomo unaotarajiwa kuanza Julai 18.
“Naagiza wanafunzi wote kuripoti katika shule walizopangiwa kwa wakati. Endapo mwanafunzi atachelewa kuripoti kwa zaidi ya wiki mbili kuanzia tarehe ya mwisho ya kuripoti, nafasi yake itachukuliwa na mwanafunzi mwingine aliyekosa nafasi,” alisema Majaliwa ambaye pia ni Mbunge wa Ruangwa, Lindi.
MWANANCHI
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe ameamua kutoa ufafanuzi wa sakata la mabilioni kutoka Libya ambayo amekuwa akihusishwa nayo, akieleza kuwa fedha zote zilizotolewa kwa amri ya mahakama ni mkopo na hazikuchotwa kama ilivyokuwa kwenye kashfa za Epa au Escrow.
Membe amekuwa akihusishwa na fedha hizo, Dola 20 milioni za Marekani (sawa na Sh40 bilioni) ambazo zilikuwa zimehifadhiwa katika akaunti ya Libya No.004-200-0002216-01 iliyokuwa Benki ya Rasilimali Tanzania (TIB).
Kwa mujibu wa waraka alioutoa jana kwa vyombo vya habari kuhusu fedha hizo, Membe alisema Serikali ya Libya na Tanzania zilitia sahihi mkataba wa nyongeza (Addendum to the Dept Swap Agreement) ambao ulizungumzia, pamoja na mambo mengine, matumizi ya fedha hizo.
Mkataba huo wa nyongeza unatamka katika kifungu No.4.02, kwamba, fedha hizo zikopeshwe kwa mwekezaji aliyeteuliwa na Libya, ambaye ni kampuni ya Meis Industries Limited kwa ajili ya mradi wa ujenzi wa kiwanda cha Saruji mkoani Lindi.
“Ni mkopo uliotolewa kwa Kampuni ya Meis kwa mujibu wa Mkataba wa Makubaliano (Investment Agreement) wenye masharti ya kibenki. Na Masharti hayo ya kibenki yanamtaka mwekezaji kuweka dhamana, kulipia riba, kuwekewa muda wa kurudisha mkopo, na anawekewa hatua za kuchukuliwa endapo mwekezaji huyo atashindwa kulipa mkopo,” Membe.
“Kwa lugha nyingine, kampuni ya Meis ikishindwa kulipa mkopo huo, itafilisiwa mali zake na TIB itarudishiwa fedha zake. Iacheni benki ifanye kazi yake. Mkopo unageukaje kuwa ufisadi?”
Membe alisema yeye hana kampuni hapa nchini, hana ubia na kampuni yoyote, pia hana hisa katika kampuni ya Meis na hajafaidika na mkopo huo ambao unasimamiwa na TIB.
“Ndiyo maana uvumi kuwa nahusika na ufisadi wa mabilioni ya Libya hauna mashiko kabisa. Baadhi ya wanasiasa wenzangu wanajua ukweli wote huu, lakini kwa makusudi wanaamua kuwafanya watu waamini,” Membe.
Anasema ujenzi wa kiwanda cha saruji cha Lindi unaendelea vizuri na mitambo yote inayotakiwa katika ujenzi huo imeshawasili.
“Asilimia 45 ya ujenzi wa kiwanda hicho umekamilika na ni mategemeo ya kampuni ya Meis kuwa kiwanda hicho kitakamilika ifikapo Desemba mwaka huu wa 2015,” anasema.
Alisema kumbukumbu zinaonyesha mambo mawili, kwamba, kabla ya Serikali ya Libya kutia sahihi nyongeza hiyo ya mkataba iliyotaka fedha zikopeshwe kwa Meis, upembuzi yakinifu wa mradi husika ulifanywa na Libya kupitia vyombo vyake, walishajiridhisha juu ya ubora wa mradi huo.
Pili alisema baada ya kutia sahihi nyongeza ya mkataba, serikali ya Libya kupitia ubalozi wake hapa nchini iliendelea kusisitiza kwa maandishi kwamba Serikali ya Tanzania iharakishe mchakato wa kuwezesha fedha hizo zikopeshwe kwa mwekezaji waliyemteua ili mradi huo muhimu usiendelee kuchelewa, na pia fedha ziingie katika mzunguko kwa manufaa ya Watanzania.
NIPASHE
Mbunge wa Songea Mjini, Emmanuel Nchimbi, ametamka rasmi kuwa azma ya kuomba ridhaa ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) kuwania urais katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka huu.
Taarifa ya Nchimbi iliyopatikana kupitia ukurasa wake kwenye mtandao wa kijamii jana ilieleza kuwa, baada ya kuwa katika shinikizo kubwa kutoka kwa viongozi na wananchi waliomuamini ili agombee nafasi hiyo, amemua kutogombea.
“Mpaka  jana waliochukua fomu wamefikia 41, nimewaangalia wote waliochukua fomu na nimeridhika kuwa hatutaweza kumkosa Rais bora miongoni mwao, hivyo nimeamua kutogombea,” alisema.
Aliongeza, “Nimefanya uamuzi huu nikiamini kwamba bado ninayo fursa ya kuwatumikia Watanzania na kuleta maendeleo kwa namna nyingine.”
Nchimbi ambaye ni miongoni mwa watu waliokuwa wakitajwatajwa kutaka kuwania urais kupitia CCM katika taarifa yake hiyo aliwaomba radhi waliomshawishi, waliomwamini na kutarajia kuwa angegombea nafasi hiyo ya juu katika utawala wa nchi.
Nchimbi anatajwa kama mwanasiasa kijana mzoefu wa CCM akiwa amekuwa mjumbe wa Kamati Kuu kwa zaidi ya miaka 10 pia akiwa Mwenyekiti wa Vijana wa CCM kwa vipindi viwili na sasa mjumbe wa  Nec.
Kwa kauli ya Nchimbi ni kama ametangazia dunia kwamba kuna timu anaiunga mkono ingawa hajawa tayari kuitangaza.
Wakati huo huo, Nchimbi anakibarua kigumu cha kuamua jimbo atakalogombea mwaka huu kati ya jimbo lake la sasa la Songea Mjini na lililokuwa likishikiliwa na Maraehemu John Komba aliyefariki dunia Aprili, mwaka huu la Mbinga Magharibi.
Nchimbi aliwaacha njiapanda wapiga kura wa jimbo hilo baada ya kusema hajajua atagombea jimbo gani kati ya hayo mawili.
NIPASHE
Kada wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), anayeomba kuteuliwa na chama hicho kugombea urais, January Makamba, amesema mgombea  urais ‘anayemwaga’  fedha na kufanya ‘mbwembwe’ ili kushawishi wananchi wamchague, hafai kuiongoza Tanzania.
Aidha, Makamba amesema ikiwa atafanikiwa katika nafasi anayoiomba, atahakikisha anasimamia ujenzi wa reli kutoka Mtwara hadi Ruvuma pamoja na kufufua bandari.
Amesema ujenzi wa reli ni muhimu kwa kuwa utasaidia kurahisisha usafirishaji wa mazao na mizigo mingine katika mikoa mbalimbali ya Tanzania.
Alisema Bandari ya Mtwara imesahaulika kwa kipindi kirefu na inarudisha nyuma maendeleo ya mikoa ya Kusini ambayo  ilisahaulika miaka ya nyuma.
Makamba aliyasema hayo jana mjini hapa alipokuwa akisaka wadhamini ili kumwezesha kupata sifa ya kufikiriwa kuteuliwa na CCM kugombea urais.
“Mtu anayemwaga fedha na kuonyesha mbwembwe nyingi, hafai kuiongoza nchi kwa kuwa akiingia Ikulu hatalisaidia taifa,”.
Alisema zao la korosho ni lazima liwafaidishe wananchi wa Mtwara kwa kuwa katika kipindi kirefu wakulima wamekuwa wakipunjwa kwa kupewa bei ndogo.
Umati mkubwa uliokuwa ukimsikiliza Makamba, ulilipuka kwa shangwe baada ya kusikia kauli za matumaini hususani namna atakavyosaidia wananchi kunufaika na zao la korosho na ujenzi wa miundombinu.
Kuhusu zao la korosho, Makamba aliahidi kufufua viwanda vya kubangulia zao hilo ili kulipa thamani na kuachana na utaratibu wa sasa.
Kwa sasa zao la korosho linabanguliwa nje ya nchi, hatua ambayo imekuwa ikilalamikiwa na wakulima kwamba inawakandamiza kwa miaka mingi na kuwafanya kuiuza kwa bei ya kutupa.
HABARILEO
Kijana mpya wa Arsenal, Petr Cech amepokea vitisho kibao vya kutaka kuuawa kutoka kwa mashabiki wa Chelsea kufuatia kukamilika kwa mpango wa kutua Emirates kwa dau la pauni milioni 10.
Mashabiki walituma vitisho hivyo katika mtandao ya kijamii kupitia ukurasa wake waTwitter wakionyeshwa kukerwa na kitendo cha kipa huyo kuhamia kwa mahasimu wao wa jiji la London, Arsenal.
Mashabiki wa Chelsea wameonekana kutofurahishwa na uamuzi huo wa Cech kuhamia katika klabu nyingine ya London licha ya mchezaji huyo wa kimataifa kuichezea klabu hiyo kw amafanikio makubwa wakati wa kipindi chake cha miaka 11 hapo Stamford Bridge.
Watumiaji wa Twitter walimbatiza Cech jina la msaliti na kumuita nyoka wakati wengine wakisema Cech amekufa huku sura yake wakiwa wameivalisha kinyago cha sura ya nyoka.

No comments:

Post a Comment

advertise here