Friday 24 July 2015

NCHINI KENYA ULINZI NI WA KUFA MTU KILA KONA NI MAKACHELO WA MAREKANI

LAYIII

Gari na helikopta zisizopenya risasi.

Ni Obama kila kona! Muda wowote kuanzia leo wananchi wa Kenya watashuhudia kutua kwa Rais wa Marekani, Barack Hussein Obama, nchini humo huku stori kubwa ikiwa ni ulinzi uliowekwa kwa hofu ya kundi ‘haramu’ la ugaidi la Alshabaab, Ijumaa linakupeleka hadi kwa majirani zetu hao.

Ziara ya Obama ambaye ana asili ya Kenya kutokana na baba yake, Hussein Obama kuwa ni raia wa Kenya, itakuwa na ulinzi ambao hata mwenyeji wake, Rais Uhuru Kenyatta hana.
VIKOSI VYA ULINZI
Habari kutoka nchini humo zilidadavua kwamba, vikosi vya ulinzi vya Marekani, CIA, FBI na kile cha siri cha Secret Service vilitua nchini humo miezi kadhaa na kuungana na majeshi ya Kenya ili kuweka mambo safi.
Meli iliyobeba ndege za kivita.
MANOWARI ZA KIVITA
Ilielezwa kwamba, meli na manowari za kivita vimepiga kambi eneo lote la pwani ya nchi hiyo katika Bahari ya Hindi, lengo likiwa ni kuimarisha usalama wa kiongozi huyo mkubwa duniani pamoja na jopo la wafanyabiashara atakaoandamana nao.
B52 YAEGESHWA PWANI
Ilielezwa kwamba, jeshi la kwenye maji la Marekani limejikita Bahari ya Hindi kwenye ukanda wote wa Afrika Mashariki kujiandaa kuzuia shambulizi la kivita wakiwa na silaha nzito ndani ya ndege ya B52 ambayo imeegeshwa pwani ya nchi hiyo.
KAMERA, SATELAITI ZAFUNGWA
Ilisemekana kwamba, Jeshi la Kenya wameweka doria kwenye Jiji la Nairobi ambalo limetulia tuli huku likimulikwa kwa kamera maalum na satelaiti za kijeshi, barabara kufanyiwa usafi na nyingine kufungwa huku bendera za Kenya na Marekani zikiwa zimepamba Jiji la Nairobi.
AIR FORCE ONE
Imedadavuliwa kwamba, Obama atatua na ndege ya Rais wa Marekani ya Air Force One aina ya Boeing 747-200B kisha atapokelewa na gari analotumia Marekani ambalo lilitangulia kuwasili Kenya.
UWANJA WA NDEGE
Ilielezwa kwamba, kwenye Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Jomo Kenyatta atakaotua Obama, kumejaa ndege za Jeshi la Marekani na hauruhusiwi kutumiwa na ndege nyingine za biashara.
Hali ndivyo ilivyo kwa viwanja vingine pamoja na bandari, hakuna biashara inayoendelea hadi kiongozi huyo amalize ziara yake nchini humo.
Rais wa Marekani, Barach Obama (kushoto), mkewe Michelle Obama (kulia) na katikati ni Rais wa Kenya, Uhuru Kenyatta.
MAMLAKA YA ANGA
Ilielezwa kwamba, Mamlaka ya Anga ya Marekani na Makao Makuu ya Jeshi hilo Pentagon wanafanya kazi kama siafu kuhakikisha anga lote lipo shwari.
Kuna taarifa kwamba, wafanyakazi wote serikalini wasiohusika na usalama na ziara hiyo watakuwa miguu atakapowasili Obama kwani hawataenda kazini.
Kuhusiana na ulinzi wa Kenya, hata nchi za Tanzania, Somalia, Eritrea, Uganda, Rwanda na Burundi nazo zinamulikwa kusije kukatokea lolote.
Rais wa Kenya, Uhuru Kenyatta.
KILICHOMLETA
Akiwa nchini Kenya, Obama atafanya mkutano na Rais wa Kenya, Uhuru na baada ya hapo wawili hao watahudhuria Kongamano la Ubunifu wa Kibiashara Ulimwenguni la 2015 linalofanyika kwenye mji mkuu wa nchi hiyo, Nairobi.
Hii itakuwa ziara ya tatu ya Obama Afrika baada ya mwanzo kutembelea Ghana, baadaye Senegal, Afrika Kusini na Tanzania.
Kikundi cha wapiganaji cha Al-shabaab.
MAUAJI YA AL-SHABAAB
Ulinzi huo umekuja kufuatia matukio ya mauaji ambayo yamekuwa yakifanywa na Al-shabaab ambao walihusika na mauaji ya wanafunzi 148 katika Chuo Kikuu cha Garissa na shambulizi la mwaka 2013 la Jengo la Biashara la Westgate ambapo takriban watu 67 waliuawa.
Al-shabaab wamekuwa wakifanya mashambulizi ya mara kwa mara kwenye maeneo mbalimbali ya Kenya yaliyo karibu na mpaka wa Somalia, wakidai lazima vikosi vya Kenya viondoke nchini Somalia ndiyo maana Marekani wameamua kuweka ulinzi mkali kuliko ule wa Tanzania alipotua Obama mwaka 2013.
KIJIJINI KOGELO
Wakati hayo yakiendelea, inaelezwa kwamba, wakazi wa kijiji anakotoka mzazi wa Rais Obama, Kogelo, Magharibi mwa nchi hiyo, wanaamini kuwa kiongozi huyo atawatembelea kijijini hapo hivyo kwao ni hatua kubwa kwani atazidi kuwaboreshea maisha.
Kogelo ni kijiji kidogo alikozaliwa mzee Hussein Obama. Kijiji hicho hakikuwa kikijulikana wala kuwa na huduma muhimu kama maji na umeme, kama vijiji vingine nchini humo, hadi pale Barack Obama alipochaguliwa kuwa seneta ambao mwaka 2006 alifika kijijini hapo na kusaidia mambo mengi. Hivi sasa kijiji hicho kina umeme, barabara ya lami na shule.
Obama na Bibi yake.
KWA MARA YA KWANZA
Obama amepanga pia kutembelea Makao Makuu ya Umoja wa Afrika yaliyo Addis Ababa, Ethiopia ikiwa ni ziara ya kwanza kwa Rais wa Marekani kuzuru umoja huo tangu kuasisiwa kwake.

No comments:

Post a Comment

advertise here