Wednesday 30 March 2016

VIJUE VIDONDA VYA TUMBO KWA MAMA MJAMZITO

Vidonda vya tumbo kwa mama mjamzito
 
Vidonda vya tumbo kwa mama mjamzito
VIDONDA VYA TUMBO KWA MAMA MJAMZITO
Mwanamke mjamzito anaweza kupata vidonda vya tumbo kabla au baada ya ujauzito. Hata hivyo tafiti nyingi zinathibitisha idadi ya wanawake wajawazito wanaopatwa na vidonda vya tumbo kwa sasa ni ndogo sana.
Umakini unahitajika sana katika kumchunguza mama mjamzito ili kuelewa nini kitakuwa ndiyo chanzo cha vidonda vya tumbo kwake.
Mwanamke ambaye ulikuwa unaumwa vidonda vya tumbo hata kabla ya kushika ujauzito unaweza kuendelea kutumia baadhi ya dawa rafiki (hasa zitokanazo na vyakula na mimea) za kutibu au kuzuia dalili za
vidonda vya tumbo hata baada ya kuwa umepata ujauzito.
Kwa kawaida, kila dawa huwa na matokeo ya aina mbili yaani matokeo chanya (uponyaji) na matokeo hasi (uharibifu) na matokeo hasi yanapozidi huweza kusababisha hata kifo.
Moja ya matokeo hasi ya matumizi mabaya ya dawa za kutibu vidonda vya tumbo kwa kina mama wajawazito ni pamoja na mtoto kuzaliwa kilema, mtoto kufa tumboni na hata kifo kwa mama.
Wakati wa ujauzito, mama mjamzito anaweza kutokewa na kiungulia mara kwa mara na hata kiasi cha asidi kuongezeka mwilini. Ni wakati huu mwanamke anaweza kuanza kutafuta matibabu kwa ajili ya vidonda vya tumbo na ndipo umakini mkubwa unapohitajika.
Hivyo, dawa rafiki, yaani dawa ambazo hazina madhara hasi mengi ndizo zitumike kwa ajili ya mama mjamzito hasa katika kipindi cha majuma 10 ya kwanza ya ujauzito.
Licha ya kwamba dalili za vidonda vya tumbo hutoweka wakati wa ujauzito kwa wanawake wengi, baadhi ya wanawake hulalamika maumivu ni makali. Hii kwa kawaida hutokea kwa wanawake ambao maumivu ya vidonda vya tumbo yalikuwa makali walipokuwa si wajawazito.
Kama nilivyosema hapo juu, kina mama wengi wanaweza kujihisi wamepona kabisa vidonda vya tumbo wakati wanapata ujauzito au wakati wote wa kipindi cha ujauzito. Ingawa baadhi yao hutokewa na maumivu makali hata wakati wa ujauzito, na hii inatokea kwa wale ambao hata kabla ya kupata ujauzito walikuwa wakipatwa na maumivu makali hivyo hivyo.
Hivyo bado nashauri wakati huu wa ujauzito mama apewe dawa rafiki tu hasa zile zitokanazo na vyakula na mimea hadi hapo atakapojifungua. Na wakati huo huo kuwa makini kutokutumia vyakula au vinywaji vyenye asidi nyingi. Hapo chini kuna link ya post inayojadili vyakula na vinywaji anavyotakiwa na asivyotakiwa kula mtu anayesumbuliwa na vidonda vya tumbo, isome hiyo kwa maelezo zaidi.
Kwa kawaida vidonda vya tumbo huzalisha dalili chache pindi tumbo linapokuwa halina kitu, inashauriwa mama mjamzito asikae muda mrefu bila kula chakula na ale mlo mdogo mdogo ili chakula kiendelee kukaa tumboni.
Mama mjamzito pia aepuke kula kupita kiasi kwa sababu kula kupita kiasi huchochea uzalishwaji wa asidi nyingi. Kadharika, chakula kinapokuwa kingi tumboni hulifanya tumbo kujitandaza sana, na hatimaye kuchokoza vidonda.
Mama mjamzito aepuke kunywa maziwa. Watu wengi hudhani kwa kuwa maziwa hutumika kumpatia mtu mwenye tatizo la sumu mwilini, basi yanaweza pia kudhibiti kiasi cha asidi tumboni yakitumika kwa mtu mwenye vidonda vya tumbo. Hili si kweli, tafiti za kitaalamu za hivi karibuni zinathibitisha kwamba maziwa yasitumike kwa mtu mwenye tatizo la vidonda vya tumbo.
Mhimu kuliko yote ni kutambua kuwa vidonda vya tumbo vinatibika kabisa, unachohitaji ni kuufahamu hasa ugonjwa wenyewe huletwa na nini hasa mwilini na namna ya kuishi kwa maana ya kula na kunywa na hatimaye uponyaji ufanyike. Dawa peke yake bila kujuwa nini ule na kunywa hazitasaidia uponyaji wa vidonda vya tumbo.
Na mpaka hapa tumefikia mwisho wa somo hili kuhusu VIDONDA VYA TUMBO ambalo tumekuwa tukilijadili taratibu kipengele hadi kipengele kuanzia 06/06/2015. Ninaomba sasa uniambie baada ya vidonda vya tumbo, ni ugonjwa gani mwingine unapenda tuanze kujifunza na kuujadili taratibu kama tulivyofanya kwa vidonda vya tumbo. Ugonjwa utakotajwa na wengi zaidi ndiyo huo tutakaouanza kuujadili kuanzia post zijazo.

Umeipenda makala hii? Jiunge kwa email upokee makala mpya zinapoandikwa hapa. Andika jina lako kamili na email unayoitumia kila mara kisha bonyeza kitufe chenye neno Subscribe. Hakikisha unaithibitisha (confirm) hiyo email yako kwa link nitakayokutumia ndipo utatumiwa makala.

No comments:

Post a Comment

advertise here