Wednesday 2 March 2016

KIJUE KISA CHA WABUNGE WA UKAWA KUSAKWA KILA KONA

LAYIII


Wakati baadhi ya wabunge wa upinzani wakishikiliwa na polisi ama kutafutwa kutokana na chaguzi kile kinachoelezwa ni vurugu kwenye chaguzi za Meya na wenyeviti wa halmashauri zinazoendelea, wale waliotolewa Bungeni kwa nguvu Januari 27, wote wametakiwa kufika Dar es Salaam  wahojiwe.
Mpaka sasa Mbunge wa Kawe, Halima Mdee, anashikiliwa na polisi kwa kile kilichoelezwa ni vurugu zilizotokea baada ya uchaguzi wa Meya wa Dar es Salaam kuahirishwa Februari 27, mwaka huu.
Mbali na Mdee ambaye jana ilidaiwa kuwa polisi walifanya ukaguzi nyumbani kwake pamoja na ofisini kwake huku kile wanachokitafuta kikiwa hakijulikani, Mbunge wa Ukonga, Mwita Waitara (Chadema) na wa Ubungo, Saed Kubenea, pia inadaiwa wanatafuwa kwa sababu ya vurugu hizo.
Mbunge mwingine wa Chadema anayetafutwa na polisi ni Peter Lijuakali, wa Kilombero, aliyedaiwa kukamatwa kwa kile kilichoelezwa ni kuingia kwenye mkutano wa uchaguzi wa Mwenyekiti wa Halmashauri ya Kilombero uliofanyika jana, ambapo yeye alisema ni mjumbe huku wasimamizi wakisema siyo mjumbe.
MBOWE
Kiongozi wa Upinzani Bungeni, Freeman Mbowe, ambaye pia ni Mwenyekiti wa Chadema, jana aliwaambia waandishi wa habari kuwa wabunge na madiwani wa kutoka vyama vinavyounda Ukawa, wanadhalilishwa na kunyanyaswa kila kona nchini na kwamba hizo ni juhudi za kurudisha nyuma kazi kwa viongozi hao.
Mbowe alisema baadhi ya wabunge kutoka kwenye vyama vinavyounda Ukawa, wamepokea barua kutoka kwa Katibu wa Bunge, Dk. Thomas Kashilillah, ili kuonana na Kamati ya Haki, Madaraka na Kinga ya Bunge.
Alisema kosa linalowakabili ni kubishana na Mwenyekiti wa Bunge, Andrew Chenge, kuhusu usitishwaji wa matangazo TBC kwenye mijadala ya Bunge.
Akizungumzia kamatakamata ya wabunge wao, alisema licha ya Mdee kukamatwa tangu juzi na kulala rumande, polisi walifika nyumbani kwa Mbunge huyo wa Kawe na kupekua nyumba yake, hatua ambayo ameitaja ni udhalilishaji.
“Kumekuwa na mizengwe tangu awali katika maeneo hayo, lakini Umeya wa Jiji, CCM inafahamu kuwa kuna ufisadi mkubwa kuanzia, nyumba za jiji, viwanja, usafiri wa Kampuni ya Usafishaji Dar es Salaam (Uda) pamoja na kandarasi nyingi za kutoa huduma za kijamii ikiwamo maji na nyinginezo,” alisema Mbowe.
Alisema mbali na Mdee, Mbunge wa Ukonga, Waitara na baadhi ya madiwani wao wanatafutwa na polisi na wengine wameshikiliwa na jeshi hilo.
Alisema mbali na kuwashikilia wabunge hao, kuna njama za kuwawekea dawa za kulevya ili wabambikiziwe kesi nyingine.
Mbowe aliwabebesha lawama viongozi wakuu wa nchi kuhusika na mambo hayo.
“Hana mamlaka ya kuvunja sheria kwamba wananchi wasipige kura na ameonyesha udhaifu Dar es Salaaam, Kyerwa, Kilombero na maeneo yote yaliyo na Ukawa wengi,” alisema.
Alisema watumishi ambao wanasababisha uchaguzi wa meya kukwama akiwamo, Katibu Tawala wa Mkoa (RAS) wa Dar es Salaam, Theresia Mmbando, achukuliwe hatua na si kuwakamata viongozi wa Ukawa, kwani RAS alizuia uchaguzi kufanyika, huku ikifahamika kuwa zuio lililotumika ni batili.
Aidha, alisema kuna mkakati wa kuvunja baraza la madiwani ili kuunda Tume kwa lengo la kuvunja nguvu ya Ukawa kupitia baraza hilo.
Mbowe aliyasema hayo jana jijini Dar es Salaam kabla ya kufanyika kwa kikao cha Kamati Kuu ya chama hicho, ili kujadili ajenda mbalimbali ikiwamo suala la kukamatwa kwa wabunge na madiwani, uchaguzi wa umeya wa jiji la Dar es Salaam na wenyeviti katika halmashauri ikiwamo Kyerwa Mkoa wa Kagera na Kilombero mkoani Morogoro.
KUBENEA
Kubenea alipotafutwa na gazeti hili, alisema japo hajapata wito rasmi kutoka kwa jeshi hilo, lakini amesikia kwamba anatafutwa na kwamba yuko tayari kwenda endapo atapata barua rasmi ya wito huo.
“Ninaomba wananchi wanielewe, mimi siogopi polisi, nimesikia bado wananitafuta, nataka  aniite `officially’  nitakwenda. Nafahamu kwamba kuna njama ambazo wamepanga kwa ajili ya kunibambikia kesi kwa sababu wameshajua kwamba ninafahamu mambo mengi ambayo wanajua nikienda bungeni nitawalipua,” alisema na kuongeza:
“Niko tayari kwa lolote, siogopi, nitahakikisha ninaendelea  kutetea ukweli na haki za wanyonge, hata kama watanibambikia kesi, mimi naamini  Mungu yupo upande wangu atanitetea, kama kosa langu ni kusimamia ukweli wasifikiri kwamba wanaweza kuniziba mdomo kwa kunikandamiza. Kwa nini wanaacha kuhangaika na watu wanaodanganya badala yake wanahangaikana sisi ambao hatuna hatia.”
KAULI YA BUNGE
Kwa upande wake, Naibu Katibu wa Bunge, John Joel, alisema ni kweli kwamba baadhi ya wabunge wa waliotolewa kwa nguvu Bungeni wakati kutokana na kupinga Televisheni ya Taifa (TBC), kutorusha moja kwa moja mijadala ya Bunge wametakiwa kufika Dar es Salaa ili wakahojiwe na Kamati ya Maadili ya Bunge.
Alisema kamati hiyo inatarajia kukaa Machi 7 hadi 11, mwaka kuhoji wabunge hao ambao alisema idadi yake haijui kwa sababu bado hajawasiliana na itakuwa na kazi ya kuwahoji wabunge hao ambao walitolewa kwa amri ya Mwenyekiti wa Bunge, Chenge.
“Ni kweli wabunge wa upinzani wameandikiwa barua ya wito wa kwenda kuhojiwa, lakini sifahamu idadi kamili ya wabunge hao kwa sababu sijawasiliana na Mwenyekiti wa kamati hiyo,” alisema.
Alisema sababu ya wabunge hao kuhojiwa ni kutokana na kutolewa nje kwa amri ya Mwenyekiti wa Bunge na siyo kutoka kwa hiari yao.
“Kuna mambo mawili mnayochanganya. Kuna wale waliotoka wenyewe kwa hiari yao, hawawezi kuhojiwa, lakini kwa wale wanaotolewa na Spika wa Bunge, Sheria za Kanuni za Bunge zinaeleza kuwa watatakiwa kuhojiwa na Kamati ya Maadili,” alisema Joel.
Alisema kanuni ya 71 kifungu cha 1 na 2 kinaeleza kuhusu Kamati ya Maadili kuwaita na kuwahoji wabunge waliotolewa nje na Spika.
“Maana Spika anapowatoa nje wabunge ili kutuliza vurugu, ina maana anarejesha Bunge na kutoa taarifa ya kupeleka jambo hilo Kamati ya Maadili,” alifafanua.
KAMATA KAMATA MOROGORO
Mkoani Morogoro, Mbunge wa Kilombero (Chadema),  Lijualikali, anashikiliwa  na Polisi kwa kile kilichoelezwa ni kutokana na kukaidi agizo la kutoingia katika uchaguzi huo la Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Kilombero.
Mbali ya mbunge huyo, pia dereva wake, Steven Mdata na dereva wa Mbunge wa Viti Maalum Mkoa wa Morogoro, Devota Minja (Chadema), aliyetambuliwa kwa jina moja la  John, alikamatawa.
Katika sakata la Mbunge Lijualikali ambaye alifika eneo la tukio saa 3:30 asubuhi na kuzuiwa na askari waliokuwa wakilinda na kumueleza kuwa haruhusiwi kuingia ukumbini kwa kuwa hawana taarifa zake, huku mbunge huyo akidai yeye ni Mbunge na ana kibali cha kuhudhuria mkutano huo kwa mujibu wa sheria.
Majibizano ya Mbunge na askari hao yalidumu kwa nusu saa na hayakuzaa matunda licha ya kutaka kwenda kupata ufafanuzi wa kuzuiliwa kwake kutoka kwa msimamizi wa uchaguzi huo, lakini askari hao waliendelea na msimamo huo.
Kufuatia hali hiyo, Mbunge huyo aliamua kuingia kwenye gari lake na kuendesha mwenyewe na kuingia na  kukata uzio uliowekwa na polisi hadi katika eneo la  ukumbi kwa kasi na kushuka kutaka kuingia ukumbini.
Kabla ya kuingia, ndipo askari zaidi ya 10 walipomkamata  kwa nguvu na kumuingiza katika gari la polisi kumpeleka katika Kituo Kikuu cha Polisi Kilombero pamoja na dereva wake, Mdata na dereva wa Mbunge wa Viti Maalum, John.
Habari hii imeandaliwa na Christina Mwakangale, Mary Geofrey Dar na Ashton Balaigwa, Morogoro.
CHANZO: NIPASHE

No comments:

Post a Comment

advertise here