Monday 6 July 2015

BZMORNING TANZANIA NA MAGAZETI YA LEO 6/7/2015

LAYIII

PEPA 
NIPASHE

#MAGAZETINI JULY6…Mume kumnyonga mjamzito, wiki ngumu CCM na kompyuta yaibiwa kituo cha kupigakura


Zikiwa zimebakia siku sita kwa Chama Cha Mapinduzi (CCM) kumpata mgombea wake wa urais katika uchaguzi mkuu wa Oktoba 25, mwaka huu, kura ya maoni iliyoendeshwa na Mpango wa Utafiti na Elimu ya Demokrasia (REDET) ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, inamweka kileleni Waziri Mkuu wa zamani, Edward Lowassa, kuwa changuo la kwanza la wengi kwa kujipatia asilimia 27.0 ndani ya chama hicho.
Wakati Lowassa akiwafunika watia nia wenzake ndani ya CCM, Katibu Mkuu wa Chadema, Dk. Wilbroad Slaa, anawafunika wenzake kwenye Umoja wa Katiba ya Wananchi (UKAWA) akiwa changuo la wengi kwa asilimia 23.1.

REDET wamesema kuwa matokeo ya utafiti huo yanaweza kuchukuliwa kwa ujumla wake kama maoni ya Watanzania endapo masuala yaliyoulizwa uchaguzi ungefanyika katika kipindi cha utafiti.
“Sampuli iliyotumika katika utafiti huu kwa kiwango cha kutosha ni wakilishi na ina akisi hali halisi ya Watanzania,”  imesisitiza ripoti hiyo iliyojatwa kuwa ni maoni ya wananchi kuhusu Uchaguzi Mkuu ujao wa Oktoba 2015, mwaka huu.
Katika utitiri wa watia nia ndani ya CCM, kati ya wahojiwa 1,250 waliohojiwa, Lowassa alipigiwa kura na watu 338, wakati Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe, akipata asilimia 8.2 akichaguliwa na watu 103.
Utafiti wa REDET ulifanyika katika wilaya moja moja kwenye mikoa 25 ya Tanzania Bara baada ya wahojaji kukataliwa ruhusa ya kufanya utafiti wao katika mikoa mitano ya Zanzibar.
Utafiti huo uliokuwa umedhaminiwa na kampuni ya Business Times Limited, ulifanyika kati ya Juni 23-26, mwaka huu na kila wilaya ilikuwa na wahojiwa 50.
Kwa upande wa CCM watia nia wengine ni Mizengo Pinda nafasi ya tatu akiwa na asilimia 7.2 akichaguliwa na watu 90; John Magufuli nafasi ya nne akipata asilimia 6.6 akipigiwa kura na watu 83 na Charles Makongoro Nyerere nafasi ya tano akipigiwa kura na watu 54.
Wengine ni Mark Mwandosya nafasi ya sita akipata asilimia 3.1 akichaguliwa na watu 39; Dk. Harrison Mwakyembe nafasi ya saba akiwa na asilimia 1.4 akichanguliwa na watu 18; Frederick Sumaye nafasi ya nane akipata asilimia 1.4 akichaguliwa na watu 17; nafasi ya tisa imekamatwa na Jaji Augustino Ramadhani akiwa na asilimia 1.2 akichaguliwa na watu 15 na nafasi ya 10 amekamata Mwigulu Nchemba akiwa na asilimia 1.0 akichaguliwa na watu 13.
Wengine na idadi ya waliowachagua na asilimia zao kwenye mabano ni January Makamba nafasi ya 11 (asilimia 0.8, watu 10); Dk. Asha-Rose Migiro nafasi ya 12 (asilimia 0.7, watu tisa); Samuel Sitta nafasi 13 (asilimia 0.6. watu wanane); Lazaro Nyalandu nafasi ya 14 (asilimia 0.4, watu watano).
Pia wamo Prof. Sospeter Muhongo nafasi ya 15 (asilimia 0.4, watu watano); Balozi Amina Salum Ali nafasi ya 16 (asilimia 0.2, watu wawili); Dk. Mohammed Gharib Bilal nafasi ya 17 (asilimia 0.2, watu watatu); Stephen Wasira nafasi ya 18 (asilimia 0.2, watu 3) na William Ngeleja nafasi ya 19 (asilimia 0.2, watu wawili).
Wengine ni Balozi Ally Karume nafasi ya 20 (asilimia 0.1, mtu mmoja); Amos Siyantemi nafasi ya 21 (asilimia 0.1, mtu mmoja); Joseph Chagama nafasi ya 22 (asilimia 0.1, mtu mmoja); na Mwele Malecela nafasi ya 23 (asilimia 0.1, mtu mmoja).
Katika kura hiyo, watia nia 14 ambao wamejitosa kwenye urais kupitia CCM hawakutajwa kabisa na watoa maoni ambao ni Balozi Augustine Mahiga; Boniphace Ndengo; Eldophonce Bihelo; Godwin Mwaipopo; Dk. Hamis Kigwangalla; Dk. Hans Kitine; Joseph Chagana; Leons Mulenda; Luaga Mpina; Maliki Marupu; Mathias Chikawe; Monica Mbega; Titus Kamani na Balozi Patrick Chokala.
Kwenye kundi la Ukawa, namba mbili amechukua Prof. Ibrahim Lipumba akiwa na asilimia 13.6 akichaguliwa na watu 170; Freeman Mbowe ameshika nafasi ya tatu akiwa na asilimia 7.2 akichaguliwa na watu 90; James Mbatia amekamata nafasi ya nne akiwa na asilimia 3.2 akichaguliwa na watu 40; Emmanuel Makaidi akishikilia nafasi ya tano kwa asilimia 0.6 akichaguliwa na watu 8, huku George Kahangwa akishika nafasi ya sita kwa asilimia 0.2 akichaguliwa na watu wawili.
Swali la msingi lililokuwa linaulizwa lilisema: “Kama wewe leo ungeshirikishwa katika mchakato wa uteuzi wa mgombea urais kwa tiketi ya CCM, kati ya wanachama wake 37 waliokwishajitokeza, ungemchagua nani apeperushe bendera ya chama hicho katika uchaguzi mkuu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Oktoba 2015?”
Pia swali kwa Ukawa lilikuwa: “Kama wewe leo ungeshirikishwa katika mchakato wa uteuzi wa mgombea urais kwa tiketi ya vyama vinavyounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa), kati ya wanachama wake waliokwishakutangaza nia na wanaotarajia kutangaza nia ungemchagua nani apeperushe bendera ya Ukawa katika uchaguzi mkuu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Oktoba 2015?”
Ripoti ya REDET imesema kuwa kwa maswali yote, mhoji alitakiwa kutomtajia majina mhojiwa, bali mhojiwa aliombwa ataje jina alilonalo kichwani mwake.
NIPASHE
Hatma ya Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, jijini Dar es Salaam, kusoma au kutokusoma hukumu ya kesi inayowakabili mawaziri waandamizi wa zamani, Basil Mramba, Daniel Yona na aliyekuwa Katibu Mkuu wa Hazina, Gray Mgonja wanaokabiliwa na kesi ya matumizi mabaya ya ofisi na kuisababishia serikali hasara ya Sh. bilioni 11.7 itajulikana leo.
Mahakama hiyo imepiga kalenda kusoma hukumu hiyo mara mbili tofauti kati ya Juni 30 na Julai 3, mwaka huu kutokana na sababu tofauti ikiwamo jopo linalosikiliza kesi hiyo kutokukamilika.
Mapema Juni 30, mwaka huu saa 3:00 asubuhi, jopo la mahakimu wawili, likiongozwa na Mwenyekiti Jaji John Utamwa na Samu Rumanyika walipiga kalenda kusoma hukumu hiyo hadi Julai 3, mwaka huu baada ya mjumbe Hakimu Saul Kinemela kuwa na udhuru wa kikazi.
Hata hivyo, Julai 3, mwaka huu mahakama hiyo kwa mara ya pili, ilipiga kalenda kusoma hukumu hiyo kwa madai kuwa Mwenyekiti wa jopo, jaji Utamwa ni mgonjwa.
 Katika kesi hiyo washtakiwa hao pia wanadaiwa kutumia madaraka vibaya na kutoa msamaha wa kodi kwa Kampuni ya Alex Stewart (Assayers), Government Business Corporation kufanya ukaguzi wa madini ya dhahabu nchini.
Kwa mujibu wa sheria ya makosa ya jinai, kosa la matumizi mabaya ya madaraka adhabu zake ni kulipa faini ya Sh. milioni mbili au kifungo cha kati ya mwaka mmoja au miaka mitatu jela baada ya mshtakiwa kupatikana na hatia.
Katika mashtaka hayo ilidaiwa kuwa washtakiwa wakiwa watumishi wa serikali, Oktoba 10, mwaka 2003 walikaidi ushauri wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) wa kuwataka wasitoe msamaha kwa Kampuni ya Alex Sterwart (Assayers) Government Business Corporation.
NIPASHE
Mbunge wa kuteuliwa na Mwenyekiti wa Chama cha NCCR- Mageuzi, James Mbatia,  amesema hakuna Spika aliyewahi kuonyesha udhaifu katika Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kama alivyoonyesha Anna Makinda.
Amesema Makinda ameligawa vipande vipande Bunge la 10 na kutumiwa na mhimili wa utawala.
Mbatia alisema badala ya Bunge kuisimamia serikali, lakini Makinda ameshindwa kuliongoza Bunge hilo kutokana na shinikizo la mhimili wa utawala na kulazimika kufuata matakwa ya CCM na hivyo kuliongoza kwa ubabe.
Alisema tofauti na ilivyokuwa katika kipindi cha  Samuel Sitta na Pius Msekwa ambao walionyesha weledi na kuliongezea heshima Bunge, lakini Makinda ameriharibu kutokana na kuacha kusimamia Katiba ya nchi katika kuliongoza Bunge hilo.
“Siku zote mwanamke ndiye huwa ni mtu wa mwisho kuligawa Taifa, lakini limekuwa ni jambo la ajabu sana kuona mwanamke huyo ambaye angekuwa mstari wa mbele katika kuitetea nchi hii, lakini ameamua lifie mikononi mwake, hata bila kuficha ameonyesha wazi kwamba anatumika na serikali na CCM, Makinda yeye siyo kiranja wa bunge  ni mratibu tu,” Mbatia.
Aliongeza: “ Badala ya Bunge kusimamia serikali kama Mhimili unaojitegemea, limejivua kazi yake na kuwa kiungo cha serikali na inalisimamia, na ndiyo  maana hata juzi mlisikia Serikali inasema imeoliongezea Bunge siku, badala ya Bunge lijiongezee lenyewe, hii ni fedheha.”
Mbatia alisema suala la kupelekwa bungeni kwa hati ya dharura na kujadiliwa miswaada mitatu ya mafuta na gesi ni ajenda ya siri ya kutaka kuiweka gesi kama dhamana ya CCM ya kupata fedha ya uchaguzi na  kwamba hicho ni kiashiria cha kuanza kuiuza nchi rejareja.
 
“Raslimali hizi badala ya kuwa neema kwa Watanzania, sasa inakuwa balaa, watu wachache wanataka kuwaibia Watanzania, hivi unawezaje kuwekaje miswaada hii muhimu kujadiliwa kwa pamoja na kuipeleka harakaharaka hivyo, sisi tumesema hatukubali kuona hujuma hizi zinafanyika dhidi ya rasilimali na Taifa,”Mbatia.
Mbatia alisema msimamo wa Wabunge wa Umoja wa Katiba ya Wananchi (UKAWA) uko wazi, kwamba hawako tayari kujadiliwa miswaada hiyo kwa hati ya dharura na pia hawatashiriki wakati wa kuvunjwa bunge hilo Julai 9, mwaka huu.
Pia aliongeza kuwa hata wakiitwa katika meza ya maridhiano na Makinda hawatakuwa tayari kushiriki.
Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, Nape Nnauye, alipoulizwa juu ya taarifa hizo za kwamba chama hicho kina  ajenga ya siri ya kuifanya gesi kusaidia kuwa dhamana  katika uchaguzi, alijibu kwa kifupi kwamba ni uzushi.
HABARILEO
Mlinzi wa usiku katika Ofisi za Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Kalambo mkoani Rukwa, Florence Kazonde  amejinyonga baada ya kumuua kikatili kwa kumkaba koo mkewe aliyekuwa na ujauzito wa miezi tisa, Emilia Mzui.
Chanzo cha mauaji hayo kimeelezwa kuwa ni wivu wa kimapenzi. Tukio hilo limethibitishwa na Jeshi la Polisi mkoani Rukwa, majirani na ndugu wa karibu wa familia ya marehemu hao waliokuwa wanaishi katika Kitongoji cha Namlangwa mjini Matai yalipo makao makuu ya wilaya ya Kalambo.
Kwa mujibu wa Ofisa Habari wa Halmashauri hiyo, Ramadhan Juma, alikiri kuwa Kazonde alikuwa mlinzi wa ofisi za Mkurugenzi Mtendaji wa halmashauri hiyo zilizopo nje kidogo ya Mji wa Matai, lakini hakuwa mwajiriwa wa halmashauri hiyo.
“Kazonde alikuwa anatoka katika kampuni moja ya ulinzi…hakuajiriwa na Halmashauri hii,“ alisisitiza Juma.
Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Rukwa, Jacob Mwaruanda alieleza kutokuwa na taarifa za mkasa huo kwamba akizipata atazitolea taarifa.
Hata hivyo taarifa kutoka Jeshi hilo la Polisi mkoani humo limethibitisha kutokea kwa tukio hilo. “Kweli kuna hilo tukio limetokea wilayani Kalambo … taarifa zipo tayari lakini kwa kuwa mie si msemaji wa Jeshi hili siwezi kutoa maelezo zaidi ya kina lakini nikiri kuwa tukio hilo limetokea …Kwa utaratibu wa Jeshi letu ni Kamanda wa Polisi wa Mkoa ndiye msemaji na si vinginevyo.
Baadhi ya majirani na ndugu wa karibu kwa masharti ya kutoandikwa gazetini walieleza kuwa walibaini vifo hivyo baada ya kufika nyumbani kwa wanandoa hao ili kuwasabahi lakini walikuta milango ya nyumba hiyo imefungwa kwa ndani.
“..Tulihisi labda walikuwa bado wamelala lakini kila tukibisha hodi ni watoto tu waliokuwa wakiitikia …… “Mazingira hayo yalitutia mashaka makubwa tukahisi kuwa kwa kuwa mke wake siku zake za kujifungua zilikuwa zimekaribia tuliamini kuwa walikuwa wamekwenda hospitali na kuwaacha watoto wakiwa wamejifungia ndani na kushindwa kufungua milango hiyo, “ alisema mtoa taarifa.
Ilielezwa kuwa ndugu na majirani hao waliamua kufungua mlango kwa nguvu ili wawatoe watoto hao wadogo nje ambao walikuwa wawili.
Kwa mujibu wa mtoa taarifa baada ya kufungua mlango wa nyumba hiyo kwa nguvu mmoja wa watoto hao aliwaonesha ishara kuwa chumbani kwa wazazi wao kuna kitu cha kutisha ndipo walipolazimika kuingia chumbani humo na kuona mwili wa Kazonde ukiwa umening’inia darini ukiwa na kamba ya katani shingoni ambapo mwili wa marehemu mkewe ulikuwa kitandani.
“Inatisha na kusikitisha sana ….tuligundua kuwa wote wawili walikuwa wafu tukatoa taarifa mara moja katika Kituo cha Polisi hapa mjini Matai …… askari Polisi walifika na waganga ambao walifanyia uchunguzi miili hiyo na kuthibitisha kuwa Kazonde alikuwa amejinyonga baada ya kumuua mke wake kikatili kwa kumkaba koo,” aliongeza mmoja wa ndugu wa karibu.
Taarifa kutoka eneo hilo la tukio zinaeleza kuwa kwa muda mrefu wanandoa hao walikuwa wakigombana mara kwa mara ambapo mume alikuwa akimtuhumu mkewe kuwa na mahusiano ya kimapenzi na wanaume wengine na kwamba kati ya watoto wao wawili mmoja sio wake ni wa mwanamume mwingine.
HABARILEO
Kikao cha Kamati Maalumu ya Halmashauri Kuu ya Taifa ya CCM -Zanzibar kwa kauli moja imependekeza kwa Kamati Kuu jina la Rais wa Zanzibar, Dk Ali Mohamed Shein kuteuliwa kuwania tena kiti cha Rais wa Zanzibar katika uchaguzi mkuu wa baadaye mwaka huu.
Kwa mujibu wa Naibu Katibu Mkuu wa CCM, Vuai Ali Vuai, kikao hicho maalumu pamoja na mambo mengine, kilipokea na kujadili jina la Makamu Mwenyekiti wa CCM, Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Zanzibar, Dk Shein.
Kikao hicho kilichoongozwa kwa muda na Makamu wa Rais wa Tanzania, Dk Mohamed Gharib Bilal kilipokea taarifa ya jina la Dk Shein ambaye ni mgombea pekee kwa nafasi hiyo.
“Kamati Maalumu ya Halmashauri Kuu ya CCM Taifa Zanzibar kwa kauli moja inapendekeza kwa Kamati Kuu jina la mgombea wa nafasi ya Urais wa Zanzibar kuwa ni Dk Ali Mohamed Shein kuwania nafasi hiyo kwa kipindi cha miaka mitano,” Vuai.
Vuai alisema wajumbe kwa kauli moja wamependekeza jina la Shein kuwania nafasi hiyo baada ya kuridhishwa na utendaji wake unaotokana na utekelezaji wa ilani ya uchaguzi ya mwaka 2010/2015 kwa vitendo katika maeneo yote muhimu.
Alisema utekelezaji huo umeiwezesha Serikali ya Mapinduzi Zanzibar kupata mafanikio katika maeneo mbalimbali ya bajeti yake kwa mwaka wa fedha 2015-2016 ikiwemo kuweka kipaumbele kwa miradi ya jamii pamoja na maendeleo.
Akimkaribisha Dk Shein, baada ya kumalizika kwa kikao hicho, Mwenyekiti wa muda, Dk Bilal, alimkabidhi kiti, ili kuendelea na mambo mengine.
Naye Dk Shein alishukuru na kukipongeza kikao hicho, kwa kufanikisha kazi hiyo muhimu na nzito kwa mafanikio makubwa na kuahidi kuwa ataendelea kuwa mwadilifu na mwaminifu mbele ya CCM, jamii nzima ya Wazanzibari na Watanzania kwa ujumla.
HABARILEO
Mahakama ya Wilaya ya Nkasi mkoani Rukwa imemhukumu Mwenyekiti wa Kijiji cha Mbende, Alei Charles (CHADEMA) kifungo cha miaka miwili jela baada ya kukiri kumlinda mshtakiwa Wenceslaus Namwanda “Pepea” anayemiliki shamba la bangi.
Mshitakiwa Namawanda ambaye pia ni mkazi wa kijiji cha Mbende anakabiliwa na kosa la kumiliki shamba la bangi.
Hakimu wa mahakama hiyo, Adam Mwanjokolo alitoa adhabu hiyo baada ya mshtakiwa huyo mwenye miaka 30 kukiri kutenda kosa hilo mahamakani hapo .
Nimelazimika kutoa adhabu kali ili iwe fundisho kwa viongozi wengine wenye tabia kama yako (Alei)… hivyo utatumikia kifungo cha miaka miwili jela,“ Hakimu Mwanjokolo.
Awali Mwendesha Mashtaka, Mkaguzi wa Polisi, Hamimu Gwelo alidai mahakamani hapo kuwa mshtakiwa alitenda kosa hilo Mei 14 , mwaka huu katika kijiji cha Mbende , saa 3 usiku.
Ilidaiwa mahakamani hapo kuwa usiku huo wa tukio Alei aliwadanganya maofisa wa polisi kuwa mshtakiwa Namwanda hakuwa mkazi wa kijiji hicho hivyo aliwaelekeza kwa Mwenyekiti wa kijiji cha jirani.
Kwa mujibu wa Mwendesha Mashtaka, maofisa hao walithibitishiwa na Mwenyekiti wa kijiji cha jirani kuwa mshitakiwa wanayemtafuta anaishi katika kijiji cha Mbende ambapo aliongozana nao hadi nyumbani kwake.
“Maofisa wa Polisi walipofika nyumbani kwa mshtakiwa Namwanda walipobisha hodi ghafla alitoka mtu baada ya kuona askari alitimua mbio, askari walifanikiwa kumkamata na ikagundulika kuwa ni Mwenyekiti wa Kijiji cha Mbende ambapo alikiri kuwa alifika nyumbani kwa mshtakiwa na kumtaarifu atoroke kwa kuwa alikuwa akitafutwa na Polisi,” alieleza Mwendesha Mashtaka.
Akijitetea mshitakiwa huyo aliomba apunguziwe adhabu kwa kuwa ni kosa lake la kwanza. Pia ana watoto wategemezi wawili wa marehemu dada yake ambapo mama mzazi anaishi naye baada ya mumewe kufariki dunia.
MWANANCHI
Mbunge wa Mpanda Mjini, Said Arfi ametangaza kujivua uanachama wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema).
Arfi aliwaeleza wananchi wa Mpanda kuwa uanachama wake ndani ya Chadema utakoma mara tu baada ya kuvunjwa Bunge Julai 9.
Pia, alitumia mkutano huu kuwaaga wananchi wa jimbo hilo akisema hatagombea tena nafasi hiyo aliyoitumikia kwa miaka 10.
Arfi alifafanua kuwa hayuko tayari kugombea jimbo hilo kupitia chama chochote cha siasa na kauli hiyo imelenga kuondoa uvumi uliokuwa umeenea kwamba alikuwa na nia ya kugombea kupia ama ACT – Wazalendo au CCM.
Alisema amekuwa akishangazwa na kauli ambazo zimekuwa zikitolewa na baadhi ya wanachana na wapenzi wa Chadema kuwa hajafanya lolote kwenye chama hicho.
Alisema kama kuna mtu anayekifahamu vizuri chama hicho ni yeye, hivyo haoni sababu za watu kumbeza.
Alisema alikuwa ameamua kukaa kimya na kuwa akiamua ‘atamwaga mboga’ ili watu wafahamu upungufu ulioko ndani ya chama hicho.
Alisema hagombei katika jimbo hilo na kama kweli chama hicho kina nguvu, basi kilitetee, akisisitiza kuwa ana uhakika jimbo hilo litakwenda CCM kwa kuwa wananchi wa Mpanda Mjini walikuwa na mapenzi na mtu siyo chama.
Arfi aliyewahi kuwa Makamu Mwenyekiti wa Chadema kabla kujiuzulu wadhifa huo, aliwahi kuhusishwa kusuka mpango wa kumwezesha Waziri Mkuu, Mizengo Pinda kupita bila kupingwa katika kinyang’anyiro uchaguzi wa mwaka 2010 katika Jimbo la Katavi kwa kuwashawishi baadhi ya wagombea kuondoka majina yao.
Hata hivyo, Arfi amekuwa akikanusha tuhuma hizo, hali ambayo pia ilisababisha kutokuelewana na baadhi ya viongozi wenzake na kusababisha kujiuzulu nafasi yake ya umakamu mwenyekiti.
Baadhi ya wananchi waliozungumza na gazeti hili walionyesha kushtushwa na kauli ya mbunge huyo kujiondoa Chadema lakini wakasema ametimiza haki yake ya kikatiba kuchagua sehemu iliyo sahihi kwake.
MWANANCHI
Rais Jakaya Kikwete amewataka viongozi wa dini nchini kuwahimiza waumini wao kuwachagua wanasiasa wasiokuwa waovu, wasiofanana na uovu au hata kuukaribia.
Amewataka kuepuka makundi ya kisiasa na wasiwape mwanya wanasiasa wenye dhamira ovu katika kutafuta madaraka kwa thamani yoyote na wawakemee wale wanaotaka kupata madaraka kwa gharama yoyote.
Alisema hayo jana wakati wa uzinduzi wa maadhimisho ya miaka 125 tangu kuingia kwa injili katika ukanda wa Pwani ya Tanga na Milima ya Usambara uliofanyika katika Viwanja vya Mbuyukenda jijini hapa.
“Wanasiasa wanaotaka madaraka kwa njia yoyote ile, muwanyanyapae, wakatalieni kwa macho makavu, hawa si watu wema watatufikisha pabaya,”  Rais Kikwete.
Alisema hayo baada ya Askofu wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri (KKKT), Dayosisi ya Kaskazini Mashariki, Dk Stephen Munga kumweleza kwamba akiwa mkuu wa nchi anao wajibu wa kuhakikisha Taifa linavuka kwa amani na usalama katika kipindi hiki kigumu cha uchaguzi.
Rais Kikwete ambaye pia ni Mwenyekiti wa CCM, alisema katika kipindi hiki, viongozi wa madhehebu ya dini wasijiingize katika makundi ya wanasiasa kwa sababu mambo yakiharibika itakuwa hakuna pa kukimbilia.
Aliwataka viongozi wa dini watumie nyumba za ibada kuliombea Taifa livuke salama katika kipindi hiki kigumu badala ya kuwapangia vyama au viongozi wa kuwachagua.
“Tunawategemea kuwahimiza na kuwakumbusha kutumia haki na wajibu wao vizuri, muwahimize na kuwakumbusha kuwa watatakiwa kufanya mambo matatu muhimu; Kwanza, kujiandikisha, pili, kujitokeza kwenda kupiga kura na tatu kuchagua viongozi wazuri, wasiokuwa waovu, wasiofanana na uovu na kuukaribia uovu, watakaosukuma mbele gurudumu la maendeleo na kujali masilahi mapana ya jamii husika na nchi yetu.”
“Viongozi wa dini muwe kama mimi, nina wagombea wa urais 42, kama nitaonyesha kuwa upande wa mgombea yeyote kati yao, basi nitakuwa nimeharibu mchakato mzima wa uchaguzi.
“Tusiwape mwanya wanasiasa wenye dhamira ovu kuwafarakanisha Watanzania. Tuendelee kukemea matumizi mabaya ya fedha, rushwa, hila, ghiliba na hujuma katika uchaguzi. Tunapaswa kufanya hivyo tena zaidi sasa, wakati wa michakato ya ndani ya vyama vya siasa na baadaye wakati wa uchaguzi,” alisema.
Alisema hiki ni kipindi nyeti na kwamba, viongozi wa dini pamoja na Watanzania kwa ujumla wanapaswa kufahamu kuwa Tanzania haina kinga ya milele ya amani na utulivu, kama itavurugwa haitakuwa lulu ya Afrika tena kama ilivyo sifa yake.
“Tuwakemee wanasiasa wapenda madaraka kwa gharama yoyote, ambao watataka kutumia fedha kununua ushindi au ubaguzi wa rangi, kabila, dini na kadhalika, kuwabagua wapinzani wao na kujijenga kisiasa. Nawaomba msiwasikilize wala kuwaendekeza kwani mchezo wao ni mauti yetu. Wakatalieni kwa macho makavu na kwa kweli muwanyanyapae,” alisema.
MWANANCHI
Mgombea urais kupitia Chama cha Mapinduzi (CCM), Jaji mstaafu Augustino Ramadhani amewataka Watanzania kuendelea kumwombea ili mapenzi ya Mungu ya kumfanya kuwa kiongozi wa Taifa yatimie.
Jaji Ramadhani alisema hayo jana wakati wa sherehe za maadhimisho ya miaka 50 ya Dayosisi ya Dar es Salaam. Katika sherehe hizo, mgombea huyo alikuwa mgeni rasmi akiambatana na Dk Mwele Malecela ambaye pia anawania nafasi hiyo.
Jaji Ramadhani, ambaye ni mchungaji wa kanisa hilo alisema haikuwa mapenzi yake kutangaza nia ya kugombea urais, bali alipata msukumo kutoka kwa Mungu mwenyewe.
“Kila siku watu wananipongeza kwa kujitokeza kuwania urais. Ninawaambia safari bado ni ndefu, wazidi kuniombea ili mapenzi ya Mungu yatimie,”.
Kiongozi huyo alisema rushwa imekuwa tatizo kubwa nchini na kubainisha kuwa yeye anachukia na hata Mungu pia haipendi.
Alisema CCM imekuwa ikipambana na rushwa chini ya msemo wake ‘rushwa ni adui wa haki’ na kuwataka wananchi wabadilike na kuepuka rushwa.

No comments:

Post a Comment

advertise here